Friday, November 8, 2013

Kigwangalla ajipalia makaa CCM;Aitwa na Kamati ya bunge kujieleza

Mchakato wa kukusanya saini za wabunge za kutokuwa imani na Spika wa Bunge Anne Makinda, limeingia katika sura mpya baada ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, kumuweka kitimoto Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Khamis Kingwangalla, kwa zaidi ya saa tatu mjini Dodoma.

Dk. Kigwangala anakusanya saini za wabunge akitafuta kuungwa mkono katika hoja ya kutokuwa na imani na Makinda kwa madai kwamba amekuwa akikiuka kanuni za Bunge.

Hadi kufikia jana taarifa ambazo NIPASHE ilizipata ni kwamba wabunge 201 walikuwa wamekubali kusaini na kati yao 98 wanatoka CCM.Wengine ni kutoka CUF, NCCR Mageuzi na Chadema.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo zililifikia NIPASHE jana jioni, Dk.Kigwangalla aliitwa na kamati hiyo inayoongozwa na Hassan Ngwilizi kuhojiwa.

Habari zinasema kamati hiyo ilimwita Dk. Kingwangala ili kujiridhisha kama alifuata taratibu zote kabla ya kuanza mchakato huo na baada ya kujiridhisha kama kanuni za Bunge zilifuatwa, jambo hilo litapelekwa Bungeni kujadiliwa na wabunge wote.

Kwa mujibu wa Kanuni ya bunge ya 137 kifungu cha 1,2,3 mbunge akitaka kufanya jambo kama hilo anatakiwa kuandika barua kwa Katibu wa Bunge na kueleza sababu za kufanya hivyo.

Taarifa zinaeleza kuwa kabla ya kuitwa, kamati hiyo ilimwandikia samanzi Dk. Kigwangalla.

Dk. Kigwangalla aliibua hoja ya kutokuwa na imani na Spika katika kikao cha wabunge wote cha kuelezea shughuli zitakazofanywa na Bunge katika mkutano wa 13, Oktoba 28.

Mbunge huyo alihoji sababu za Makinda kumteua Andrew Chenge (CCM-Bariadi Magharibi) kuwa Mwenyekiti wa kamati ya Bajeti wakati kanuni zinaeleza kuwa wenyeviti wa kamati hizo wanachaguliwa na wajumbe wa kamati husika.

Pia anadaiwa kuvunjwa kwa kanuni kwa kuwapa posho ya Sh.430,000 kwa siku wajumbe wa kamati hiyo wakati wajumbe wa kamati nyingine hulipwa Sh. 130,000 kwa siku.

Source:Nipashe Ijumaa

No comments:

Post a Comment