Wednesday, November 7, 2012

CCM yalaani shambulio la tindikali dhidi ya Sheikh Fadhili Soraga

CCM yalaani shambulio la tindikali dhidi ya Sheikh Fadhili Soraga


Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Soraga akitolewa katika Chumba cha Huduma ya Kwanza katika Hospitali ya Mnazi Mmoja baada ya kurushiwa Tindikali na watu wasiojulikana wakati akifanya mazoezi huko katika Kiwanja cha Mwanakwerekwe.
Chama Cha Mapinduzi kinasikitishwa na kitendo cha kinyama alichofanyiwa Sheikh Fadhili Soraga cha kumwagiwa tindikali sehemu ya uso na kifuani. Sheikh Soraga ni mtu maarufu hapa Zanzibar kwani huwa anashiriki katika shughuli mbali mbali za kidini hapa nchini, yeye ni Katibu wa Mufti Mkuu wa Zanzibar. Sheikh Soraga amefanyiwa unyama huo na watu wasiojuulikana wakati akitoka kwenye mazowezi ya viungoasubuhi ya leo.

Sheikh Soraga ni miongoni mwa masheikh wachache hapa zanzibar wenye kuheshimika na kueleweka. Hivi karibuni Sheikh Soraga alitoa hutuba nzuri na fasaha kwenye sala ya Eid-Haji juu ya kuimarisha amani na utulivu katika visiwa vyetu vya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Khutba hiyo aliitoa mbele ya viongozi wakubwa wakitaifa waliohudhuria katika sala hio, miongoni mwa viongozi hao ni pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mh. Dk. Ali Mohamed Shein, Makamo wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharifu Hamadi, Rais Mstaau wa awamu ya sita wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume .a viongozi wengine kadhaa.

Siku hiyo hiyo katika Baraza la Iddi lililofanyika katika Ukumbi wa Salama Bwawani Sheikh Soraga wakati akitoa khutba ya utangulizi aliwaasa tena wazanzibari na watanzania kwa ujumla juu ya umuhimu wa amani, lakini katika hafla hiyo Sheikh Soraga alikwenda mbali zaidi kwani alitoa takwimu za hasara iliyoipata Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano, mashirikaya watu binafsi na ya Umma, taasisi za Kidini pamoja na vyama vya Siasa hasa Chama Cha Mapinduzi kufuatia vurugu mbali mbali zilizokuwa zikifanywa na Uamsho.

Vitendo vya kumwagiwa watu tindikali hapa Zanzubar vimeanza siku nyingi. Kama tutakumbuka mnamo mwaka 1995 Kada wa Chama Cha Mapinduzi ndugu Ali Mwinyi Msuko alimwagiwa tindikali na watu wasiojuulikana huko Wete Pemba, mwaka 2007 wakati zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura huko Pemba Sheha mmoja alimwagiwa tindi kali, na mwaka uliopita Ndu. Rashid Ali Juma Mkurugenzi wa Baraza la Mji wa Zanzibar nae alimwagiwa tindikali na watu wasiojuulikana na leo hii Sheikh Fadhil Soraga Katibu wa Mufti Muu wa Zanzibar nae amemwagiwa tindikali pia na watu wasiojuulikana.

Chama Cha Mapinduzi kinasema kimechoka kusikia vitendo hivi vya kinyama vya kumwagiwa watu tindikali na watu wasiokuulikana. Tunaviomba vyombo vya Dola kuwatafuta watu hawa waovu wasio na huruma na wenzao ili wakamatwe waweze kufikishwa kwenye vyombo vya Sheria, na kama Jeshi letu la Polisi uwezo wake ni mdogo wa kuuwafichua wahalifu hawa basi ni vyema wakaomba msaada kwenye vyombo vya upelelezi vya Kimataifa kama vile INTAPOL.

Mwisho Chama Cha Mapinduzi kinawaomba wananchi wote wapenda amani na utulivu kumuombea duwa Mwalimu wetu Sheikh Fadhil Soraga Mwenyezi Mungu ampe moyo wa subira yeye na familia yake na amjaalie wepesi ili apone haraka. Sheikh Soraga hivi sasa amesafirishwa kupelekwa Muhimbili kwa Matibabu zaidi.

“KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI’
MAPINDUZI DAIMA
Issa Haji Usssi Gavu
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC
Idara ya Itikadi na Uenezi
ZANZIBAR
06/11/2012

Tuesday, November 6, 2012

Mauaji ya Barlow: Mtuhumiwa alihudhuria mazishi, akamatwa na vielelezo

Mauaji ya Barlow: Mtuhumiwa alihudhuria mazishi, akamatwa na vielelezo



POLISI mjini Mwanza imebaini kuwa mmoja wa watuhumiwa wa mauaji ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, alikwenda kuaga mwili wa Kamanda huyo katika uwanja wa Nyamagana sambamba na wananchi wengine.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Lily Matola jana alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Abdallah Petro ‘Ndayi’ (32) mkazi wa Mjimwema mjini hapa ambaye anashikiliwa Polisi.
Kwa mujibu wa Kamanda Matola, Petro mbali na kutajwa kuhusika na mauaji hayo, pia anadaiwa kuwa na rekodi ya kufungwa miaka 30 jela katika gereza la Butimba kwa unyang’anyi wa kutumia silaha mwaka 2006.
Alitoka gerezani mwaka 2010 baada ya kukata rufaa Mahakama Kuu ya Tanzania. Petro pia imebainika pia kuwa ni mdogo wa mtuhumiwa wa kwanza katika kesi hiyo, Muganyizi Peter.
Vielelezo vyakamatwa
Kamanda Matola alisema mbali na kuwa na uhusiano huo, Petro na mtuhumiwa mwingine, Abdurahim Ismail Athuman ‘Dula’ (28) mkazi wa Mkudi Ghana, pia mjini hapa, baada ya kukamatwa kwa nyakati tofauti Mjimwema na Kilimahewa mwishoni mwa wiki, waliwapeleka polisi mahali walikoficha baadhi ya mali za marehemu.
Mali wanazodaiwa kuonesha polisi ni pamoja na redio ya mawasiliano ya Polisi na funguo za gari alilotumia kamanda Barlow siku ya tukio la mauaji yake.
Kamanda Matola alisema watuhumiwa waliwapeleka polisi katika shimo la majitaka kwenye maeneo ya Nyanshana, jijini Mwanza walipokuwa wameficha vitu hivyo.
Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Joseph Konyo alisema watuhumiwa baada ya kutimiza uhalifu, walitenganisha redio hiyo ya mawasiliano ili isipatikane.
“Damu ya mtu haipotei bure, hayo yote ni pamoja na Mungu mwenyewe, kwani sisi peke yetu hatuwezi, wananchi mmetusaidia sana,” alisema Kamanda Konyo.
Baada ya kuonesha polisi vitu hivyo ambavyo sasa vimechukuliwa kama vielelezo katika kesi ya mauaji ya Barlow, Kamanda Matola alisema watuhumiwa hao walipekuliwa na kukutwa pia na kadi tatu za simu za Vodacom na Airtel, simu ya mkononi, viatu vya ngozi na begi dogo.
Pia walikutwa na kofia mbili za kijeshi aina ya bereti; moja ikiwa ya Polisi na nyingine ya kampuni ya binafsi ya ulinzi, sare za kampuni ya ulinzi, mtarimbo, bisibisi, mapanga, televisheni mbili, sub-hoofer na deki.
Alisema walipohojiwa, walidai wamekuwa wakihifadhiwa na Ryoba Matiku ‘Mama Nyangi’ katika eneo la Nyakabungo Miembeni ambako mipango yote ya uhalifu imekuwa ikisukwa. Mama huyo anashikiliwa pia kwa mahojiano.
via gazeti la HabariLeo